SIASA



SLAA, MKAPA KUONGOZA MAPAMBANO ARUMERU, NASSARI, SUMARI WAPITISHWA
Na Waandishi wetu, Dar na Arusha
VYAMA vya CCM na Chadema vimetangaza rasmi vita ya kuwania Ubunge Jimbo la Arumeru Mashariki, mkoani Arusha huku vikianika majina ya makada watakaoongoza mapambano kwa ajili ya kujihakikishia ushindi.

CCM ambayo imempitisha Siyoi Sumari kuwania nafasi hiyo, imesema kampeni zake zitazinduliwa na Mwenyekiti mstaafu wa chama hicho ambaye pia alikuwa Rais wa awamu tatu, Benjamin Mkapa na Chadema itawatumia viongozi wake wa kitaifa, wakiongozwa na Mwenyekiti wake Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa.

Wakati huohuo, Kamati Kuu (CC) ya Chadema jana ilimpitisha, Joshua Nasari kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mdogo wa jimbo hilo.

Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Mbowe aliwaeleza viongozi wakuu wa chama hicho, wapenzi na wafuasi wa Chadema waliojazana eneo la Hoteli The Ice Age Usa-River, wilayani Arumeru jana kuwa wamejiandaa kikamilifu kunyakua jimbo hilo na kamwe hawatakubali hujuma zozote kutoka kwa mtu au chama chochote.

Mbowe aliyezungumza kabla ya kumkaribisha Katibu Mkuu wake, Dk Slaa kumtanga rasmi Nasari, alitamba kuwa mchakato wa kumtafuta mgombea kupitia chama hicho haujaacha nyufa wala mifarakano miongoni mwa wagombea na wafuasi wao kama ilivyotokea kwa vyama vingine vya siasa ambavyo hakuvitaja.

Alisema mara nyingi mipasuko ndani ya vyama vya siasa hutokana na mchakato wa kupata wagombea kutokana na hila za baadhi ya viongozi, wanachama au wapambe wa wagombea, hali aliyosema haijajitokeza ndani ya Chadema kutokana na mfumo mzuri unaozingatia demokrasia kwa wote bila kujali umaarufu au ukwasi wa mtu.

“Wagombea wote waliojitokeza kuchukua fomu kuomba uteuzi tumewaalika katika Kamati Kuu na wote wameridhika na ushindi na uteuzi wa mgombea mwenzao na wote watashiriki kikamilifu kwenye kampeni kuhakikisha ushindi wa chama unapatikana,” alisema Mbowe.

Akitangaza uamuzi wa Kamati Kuu, Dk Slaa, alisema kikao hicho kilichoshirikisha wabunge, mameya na wenyeviti wa halmashauri za wilaya zinazoongozwa na Chadema, kwa kauli moja kilipitisha jina la Nasari kuitikia sauti ya wananchi na wakazi wa Arumeru waliomchagua kwa kura 805 kati ya 888 zilizopigwa kwenye kura za maoni.

“Wananchi Arumeru tumesikia kauli yenu kupitia kura zenu za maoni, Nasari ni kijana wenu siyo wa Dk Slaa, Mbowe wala Chadema.

Katika kura za maoni, Nasari alimwacha mbali mgombea wenzake Anna Mghiwa aliyemfuatia kwa kupata kura 23 huku wagombea wengine wanne, wakipata kura chini ya 20.

Chama hicho pia kinaendelea kufanya tathimini ya kutumia helikopta katika kampeni zake katika jimbo hilo.

Nasari ashukuru

Akitoa shukrani mbele ya wajumbe wa Kamati Kuu ya chama chake, Nasari aliwaomba wafuasi, wapenzi na wanachama wote wa Chadema kushikamana na kuwa tayari kwa mapambano ya haki, kuhakikisha wanaibuka na ushindi mnono kwenye uchaguzi huo unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.

"Wao (CCM), najua watatumia dola na fedha, lakini sisi tusihofu kwani tuna Mungu anayetupigania kwa sababu mapambano yetu ni kudai haki dhidi ya uovu.
Kwa pamoja tukishirikiana kuondoa hofu kwani tutashinda," alisema Nasari.

CCM
Kwa upande CCM Kamati Kuu (CC) ya chama hicho jana ilimteua Mwenyekiti mstaafu ambaye pia ni Rais mstaafu wa awamu ya Tatu , Mkapa, kuongoza kampeni za kumnadi Mgombea Ubunge wa chama hicho, Siyoi Sumari katika jimbo la Arumeru Mashariki.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Halmashauri Kuu ya CCM, Nape Nnauye, alisema kikao cha kamati hiyo kilichoketi jana, kilipitisha jina la Siyoi kuwania nafasi hiyo iliyoachwa na baba yake, Jeremia Sumari aliyefariki usiku wa Januari 18 mwaka huu.
Nape alieleza kwamba, kamati hiyo pia imemteua Katibu wa Idara ya Uchumi na Fedha ya chama hicho, Mwingilu Nchemba kuratibu kampeni hizo.
Katika uchaguzi mdogo wa jimbo la Igunga ambao CCM ilishinda, Mkapa ndiye aliyefungua kampeni hizo huku, Nchemba akiratibu kuanzia mwanzo hadi mwisho.
Akizungumzia tuhuma za rushwa ambazo zimekuwa zikiripotiwa katika mchakato wa uteuzi, aliitaka Takukuru kuhakikisha wanakamata mtandao mzima uliohusika na utoaji rushwa.

Kauli ya Siyoi

Sumari, aliambia Mwananchi Jumapili kuwa kwamba pamoja na kufurahishwa na uamuzi wa Kamati Kuu ya CCM kupitisha jina lake kupeperusha bendera ya CCM wilayani Arumeru Mashariki, chama hicho kinapaswa kutoa ushirikiano wa dhati kuhakikisha kinatetea jimbo hilo.

Hata hivyo, alisisitiza kwamba changamoto zote alizozipitia katika mchakato wa uteuzi , zikiwemo tuhuma mbalimbali za rushwa ni misukosuko ya kisiasa ambayo haiwezi kuepukwa zaidi ya kukabiliana nayo.

“Nashukuru chama kwa kupitisha jina langu, lakini changaomoto zote nilizokuwa nikipitia naamini ni misukosuko tu ya kisiasa, lakini tusahau yaliyopita sasa tusonge mbele kunyakua ushindi,” alisema Sumari

UVCCM

Katika hatua nyingine Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM ) wilayani Arumeru, imefurahishwa na uamuzi uliofanywa na CC ya CCM kumpitisha Siyoi kupeperusha bendera ya chama hicho na kueleza kwamba kilio cha wanachama wa CCM wilayani humo, sasa kimesikilizwa.

Hata hivyo, wakati jumuiya hiyo ikiupokea ushindi huo kwa furaha, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru) imeendelea na kamata kamata yake ambapo safari hii ilimshikilia na kumhoji kwa muda Katibu Hamasa wa umoja huo wilayani Arumeru Mashariki, John Nyiti kisha kumwachia huru.

Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Esther Maleko alisema mbali na kilio cha wakazi wa jimbo hilo kusikika juu ya mgombea wao, umoja wao umejipanga kikamilifu kuingia ulingoni kuhakikisha ushindi unapatikana.

Hekaheka za uchaguzi wa jimbo hilo wakati zikiendelea baadhi ya makada wa CCM na UVCCM wilayani humo wameendelea kukumbwa na misukosuko baada ya viongozi wake akiwemo Nyiti kushikiliwa na Takukuru kwa tuhuma za kujihusisha na vitendo vya rushwa wilayani humo.

Nyiti alipoulizwa juu ya taarifa hizo kwa njia ya simu alikiri kukamatwa na maofisa wa Taasisi hiyo.

Kamanda wa Takukuru mkoani Arusha, Mbengwa Kasumambuto alipoulizwa na gazeti hili juu ya taarifa hizo hakuweza kukiri wala kukataa juu ya kuhojiwa kwa kada huyo na kudai kwamba wanaohojiwa na Taasisi hiyo wako wengi na wengine wanahojiwa kama mashahidi, hivyo alidai si vyema kuwataja majina kwa kuwa bado wanakamilisha uchunguzi wao.

Hali ilivyo ndani ya vyama

Makundi ya vigogo wa CCCM ambao wanajipanga kugombea Urais mwaka 2015, yametajwa kusababisha mpasuko mkubwa ndani ya chama hicho katika uteuzi wa mgombea wa Ubunge Arumeru Mashariki.

Mpasuko wa makundi hayo, inaelezwa unaweza kuchangia chama hicho kupoteza jimbo hilo.

Sumari amekuwa akiungwa mkono na kundi la Mbunge wa Jimbo la Monduli, Edward Lowassa huku wagombea wengine, walikuwa wakiungwa mkono na kundi la na vigogo wa chama hicho wanaojipambanua kuwa ni wapiganaji dhidi ya ufisadi...Soma zaidi www.mwananchi.co.tz                            

Mgombea ubunge jimbo la Arumeru Mashariki kupitia Chama Cha Mapinduzi,Sioi Sumari(kulia) akisalimiana na wajumbe wa mkutano mkuu wa jimbo hilo eneo la Usa River,wilayani Arumeru kabla ya upigaji kura za maoni za chama hicho juzi.
CCM kusuka au kunyoa


KAMATI KUU YAKUTANA LEO ARUSHA, SIYOI AFUGASHIWA TUHUMA ZA RUSHWA, TAKUKURU WATINGA RADIO YA LOWASSA
Waandishi Wetu
MVUTANO mkali umeripotiwa kutokea ndani ya kikao cha Kamati ya Siasa ya CCM, Mkoa wa Arusha kuhusu ni mapendekezo yapi yapelekwe mbele ya Kamati Kuu (CC) ya chama hicho baada ya matokeo ya kura za maoni kwa wanaowania kupitishwa na chama hicho kuwania ubunge katika uchaguzi mdogo Jimbo la Arumeru Mashariki.

Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinasema mvutano huo ulisababishwa na baadhi ya wajumbe wa kutaka kuondolewa kwa jina la mshindi katika kura hizo, Sioyi Sumari kwa madai kwamba ushindi wake wa kura 761 uliambatana na vitendo vya rushwa hivyo hafai kuwa mgombea wa CCM.

Katika matokeo ya uchaguzi uliorudiwa juzi, Siyoi aliibuka mshindi kwa kupata kura 761 ambazo ni sawa na asilimia 67.8 ya kura halali 1,122 zilizopigwa, dhidi ya asilimia 32.2 za mpinzani wake, William Sarakikya ambaye anadaiwa kwamba anapigiwa chapuo na viongozi wa CCM na Serikali katika ngazi za wilaya, mkoa na taifa.

Katika uchaguzi wa awali wa kura za maoni uliofanyika Februari 20 mwaka huu, Siyoi ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, Jeremia Sumari aliyefariki hivi karibuni, aliongoza kwa kupata kura 361 akifuatiwa na Sarakikya aliyejinyakulia kura 259.

Habari zinasema wakati kikao kikiendelea jana, mmoja wa vigogo wa Serikali ambaye ni mjumbe wa kikao hicho anadaiwa kuomba kwenda kufuata ripoti ya tuhuma za rushwa katika Ofisi za Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru), mkoani Arusha.

Baada ya muda inadaiwa kwamba alirejea na kile kilichodaiwa kuwa ni ripoti hiyo kisha kuiwasilisha mbele ya kikao akiwaonyesha wajumbe vielelezo mbalimbali vilivyopo ndani yake.

Taarifa hiyo ndiyo inayodaiwa kusababisha vuta nikuvute kutokana na baadhi kuipinga huku wengine wakiiunga mkono. Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda alipoulizwa juu ya taarifa hizo alikanusha akisisitiza kwamba kikao hicho kilikuwa ni cha siri na taarifa zake haziwezi kuzungumzwa hadharani.

Imeelezwa kwamba kutokana na mvutano huo ndani ya Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Arusha, wajumbe waliamua kwamba majina yote mawili, ya Sioi na Sarakikya yapelekwe mbele ya CC kama matokeo ya kura za maoni yanavyoonyesha yakiambatanishwa na maelezo na kile kilichodaiwa kuwa ni vithibitisho vya rushwa.

Kamati Kuu leo
Kutokana na hali hiyo ni dhahiri kwamba kikao cha Kamati Kuu  kinachokutana Arusha leo chini ya Rais Jakaya Kikwete kufanya uteuzi wa mwisho wa mgombea atakayebeba bendera katika uchaguzi huo, kitakuwa na wakati mgumu kufikia uamuzi kwa kuzingatia mambo makubwa mawili.

Kwanza kuamua kumweka pambeni Sumari kutokana na tuhuma hizo za rushwa zinazomwandama baada ya wanaodaiwa kuwa wafuasi wake kukamatwa na Takukuru lakini pili kumpitisha mgombea huyo kwa kuzingatia ushindi wa kura nyingi alizopata kwa wana CCM wenzake wa Arumeru.
Akichambua mwenendo wa kumpata mgombea wa CCM katika jimbo hilo, Mhadhiri wa Sayansi ya Siasa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Gaudence Mpangala alisema uamuzi wa wapiga kura unapaswa uheshimiwe.

“Tatizo letu Watanzania hatufuati misingi kamili ya demokrasia. Tunafuata tu matakwa ya watu binafsi. Kama kwenye kura za maoni za kwanza, Siyoi alishinda na kwa mara ya pili ameshinda, kuna haja gani tena ya kujadili jinsi ya kumpata mgombea?” alisema Profesa Mpangala na kuongeza:

“Kule tu kurudia kura za maoni ni ukiukwaji wa demokrasia. Hakukuwa na sababu za msingi za kurudia kwani mshindi alishapatikana. Hizi ni siasa za kizamani za chama kimoja. Kama wanafuata matakwa ya wakubwa kwa nini kuwe na uchaguzi? Kwa nini kampeni zipigwe kwa miezi miwili na zaidi? CCM inapaswa kubadilika na kusikiliza uamuzi wa wananchi.”

Huku akimnukuu Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye, Profesa Mpangala alisema utaratibu wa kurudia kura za maoni haupo hata kwenye Katiba ya CCM isipokuwa hutokea tu kwa matakwa ya watu fulani.

“Nape alisema japo utaratibu huo haupo, lakini hutokea tu kwa nyakati fulani. Alitoa mfano wa kinyang’anyiro cha urais ndani ya CCM mwaka 1995 ambapo Rais Kikwete alishinda, lakini ikaamuliwa kuwa kura zirudiwe na ndipo aliposhinda Mkapa.
Kimsingi kura za maoni huwa hazirudiwi. Mimi sijui kwa nini zimerudiwa huko Arumeru. Kama Sioyi alishinda na sasa ameshinda, basi hiyo ni dalili ya kukubalika kwa wananchi. Ikiwa kikao cha Kamati Kuu kitamwengua, basi tutajua kuwa CCM hakifuati misingi ya demokrasia.”
Wafanyakazi wa Lowassa
Wakati hayo yakijiri, kamatakamata ya Takukuru iliendelea  na safari hii ilianza kuwakumba pia wanahabari.

Miongoni mwa wanahabari waliothibitika kutiwa mbaroni jana ni Meneja wa Kituo cha Redio 5, Jimmy Mtemi. Kituo hicho kinamilikiwa na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa

Wana CCM wengine watatu walikamatwa kwenye msako huo wa Takukuru. Chanzo cha habari kutoka kwenye Redio hiyo kilieleza kwamba maofisa hao walitumia siku nzima ya jana kumtafuta Ofisa mmoja wa Redio hiyo, Pili Sirikwa.

“Hawa jamaa baada ya kumkosa Pili walikuja huku Njiro kilipo kituo cha redio wakamwulizia, walipoambiwa hayupo wakaondoka. Baada ya muda kupita walirudi tena sasa hapo ilionekana kuwa ni kwa ugomvi kwani mlinzi aliyekuwa getini walimsukuma na kuvamia ndani kisha kwenda moja kwa moja ofisini kwa Meneja.
“Baada ya kufika hapo walimweleza kuwa wanahitaji kuondoka naye hadi ofisini kwao kwa ajili ya mahojiano. Lakini kabla ya kuondokana naye walimpora simu zake za mkononi na kuzizima,” alidai mtoa taarifa wetu.

Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Arusha, Mbengwa Kasomambuto alipoulizwa kama ana taarifa zozote za kukamatwa kwa Meneja wa Redio 5, alisema bado hajapata taarifa hizo kwani alikuwa nje ya ofisi.

“Nipo nje ya ofisi nadhani kesho nitakuwa na taarifa sahihi,” alisema Kasomambuto.

Chadema nao leo
Kwa upande wake, Kamati Kuu ya Chadema leo pia inatarajia kufanya kikao hapa Arusha kutangaza jina la mgombea wao, Joshua Nassari kuwania kitu hicho.Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa alisema juzi kuwa kikao hicho kitafanyika wilayani Arumeru na tayari wajumbe kadhaa wamewasili Arusha.

“Wanachama wa Arumeru na viongozi wao wamekwishaamua juu ya mgombea wao na wametuletea mapendekezo yao na sisi tutatangaza mgombea,” alisema Dk Slaa.

Matokeo ya kura za maoni ndani ya chama hicho zilizopigwa Jumatano iliyopita yanaonyesha kwamba Nasari aliibuka na ushindi wa kishindo wa kura 805, sawa na asilima 90.6 ya kura zote 888 zilizopigwa akifuatiwa kwamba mbali na Anna Mghiwa aliyepata kura 23. Wagombea wengine na kura zao kwenye mabano ni pamoja na Samuel Kimutho (10), Yahane Shami (6), Antthon Musami (8), Rebecca Magwisha (12) na Goodlove Temba aliyepata kura 18.

CUF Haitakufa-Mtatiro


Kufuatia taarifa jana usiku saa mbili ITV kuwa uongozi mzima wa CUF wilayani Musoma umejiengua kwenye chama hicho,nilimpigia simu naibu katibu mkuu bara ambaye yuko ziarani,kutaka mwitiko wake na maoni dhidi ya hisia kwamba CUF kilikuwa kinakufa.Mara moja na kwa uhakika amesema CUF HAITAKUFA BALI IPO KWENYE HATUA KUELEKEA KUIMARIKA ZAIDI.Anasema ni lazima matukio haya yatokee ili kufikia kilele cha mafanikio.anasema ili mbegu iote hufa kwanza na kwamba hiki ni kipindi cha utakaso.Amewataka wana CUF kUWA WAVUMILIVU WAKATI HUU AMBAPO CHAMA KINAJIJENGA KUTOKEA NDANI.

BAVICHA Kufundisha Vijana Itikadi Ujerumani


Baraza la Vijana wa CHADEMA (BAVICHA) limekuwa na kawaida ya kutoa fursa za mafunzo ya makada wake ndani na nje ya Tanzania.

Dira ya BAVICHA ni kuona vijana ni nguvu ya mabadiliko ya kidemokrasia kwa maendeleo yao na ya taifa.

Kwa awamu hii BAVICHA limepanga kupeleka kada wake kwenye mafunzo ya wiki moja kwa wanasiasa vijana (Summer School) Berlin, nchini Ujerumani.

BAVICHA inawaalika vijana wa CHADEMA watakaopenda kushiriki mafunzo hayo kutuma barua ya maombi ya kushiriki, ikiambatana na wasifu unaojitosheleza (CV).

BAVICHA inahimiza vijana kutuma maombi kwa kuwa taarifa za waombaji zitahifadhiwa katika kumbukumbu (data bank) kwa ajili ya fursa nyingine zinazojitokeza.

Mwombaji pia anatakiwa ataje mawasiliano yake, namba ya kadi yake ya uanachama, tarehe ya kujiunga na chama na aeleze ushiriki wake ndani ya BAVICHA na Chama pamoja na matarajio yake ndani ya BAVICHA na CHADEMA kwa ujumla.

Maombi yatumwe kwa Katibu Mkuu wa BAVICHA kupitia bavicha@chadema.or.tz na nakala info@chadema.or.tz kabla ya tarehe 10/03/2012.

Dhima ya BAVICHA ni kuwezesha uwepo wa sera sahihi , uongozi bora na kujenga oganaizesheni thabiti ya vijana kwa maendeleo endelevu.

Duru ya pili ya uchaguzi Senegal yatangazwa

Macky Sall na Rais Wade kwenda kwa duru ya pili ya uchaguzi
Tume ya uchaguzi nchini Senegal imesema kuwa kutakuwepo na duru ya pili ya uchaguzi wa urais baada ya rais wa sasa Abdoulaye Wade, kushindwa kuzoa kura za kutosha kutangazwa mshindi wa moja kwa moja katika duru ya kwanza.
Bwana Wade alipata asilimia thelathini na tano ya kura zote zilizopigwa katika uchaguzi wa urais uliofanyika siku ya Jumapili. Rais huyo sasa atachuana na aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo wakati wa utawala wake Macky Sall ambaye alipata asilimia ishirini na sita ya kura zote zilizopigwa.
Hata hivyo ameelezea matumaini ya kunyakua tena uongozi wa nchi.
Awali rais Wade alibashiri kupata ushindi mkubwa katika duru ya kwanza ya uchaguzi.
Wadadisi wamesema rais Wade atakuwa na kibarua kigumu katika duru ya pili ikiwa upinzani utaungana dhidi yake.
Mpinzani wake, Macky Sall amesema yuko tayari kukabiliana na rais Wade na kuongeza kuwa upinzani umeshinda viti vingi zaidi vya ubunge.
Source:BBC 


Chadema Wamchagua Nassari Arumeru

 

Joshua Nassari
Waandishi wetu, Arusha
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimemchagua Joshua Nassari kupeperusha yake katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki, utakaofanyika Aprili Mosi, mwaka huu.

Akitangaza matokeo ya uteuzi huo, Mkurugenzi wa Bunge na Oganaizesheni wa Chadema, John Mrema alisema Nassari ameteuliwa baada ya kupata kura 805 sawa na asilimia 90.6 ya kura zote 888 zilizopigwa.

Alisema Nassari aliwaangusha Anna Mghiwa aliyeshika nafasi ya pili kwa kupata kura 23, akifuatiwa na Godluv Simba (18), Rebecca Magwisha (12), Samweli Shami (10), Anthony Mussari (8) na Yohanne Kimuto (6).
“Kura zilizopigwa zilikuwa 888 zilizoharibika ni sita na wagombea wote wametangaza kukubali matokeo,” alisema Mrema. Msimamizi wa uchaguzi huo alikuwa ni mwasisi wa chama hicho, Edwin Mtei.
Ukumbini

Mgombea Musari aliyehamia Chadema baada ya kuangushwa kwenye mchakato wa kutafuta mgombea kupitia CCM aliwaambia wajumbe kwamba, tayari alikwishafukuzwa kazi ya ukuu wa shule hivyo aliomba wajumbe wampigie kura kupeperusha bendera ya chama hicho kikuu cha upinzani nchini katika uchaguzi huo.

Kauli ya mgombea huyo ilimfanya mmoja wa wajumbe kutoka kata ya Maji ya Chai kumhoji iwapo hatahama tena Chadema akikosa kura katika uchaguzi huo wa jana, naye akaahidi kushirikiana na wana Chadema wenzake kutafuta ushindi wa chama chake hicho.

Awali, mzee Mtei alisema chama hicho kinahitaji wabunge wenye kuendesha na kutekeleza sera zinazojibu mahitaji ya
wananchi na jamii wanayoongoza kwa kuhakikisha rasilimali za taifa zinawanufaisha wananchi wote bila kujali tofauti miongoni mwao.

“Hivi sasa wananchi wengi wanakula mlo mmoja kwa siku sababu hawawezi kumudu gharama ya milo miwili na hili linasababishwa na usimamizi na uongozi mbovu wa Serikali ya CCM,” alisema Mtei.

Aliwaasa wana Arumeru kupuuza rushwa inayodaiwa kuwa imeanza kusambazwa sehemu mbalimbali za jimbo hilo na wanaodaiwa kuwa viongozi au wanachama wa CCM na kuchagua kiongozi wanayeamini kuwa atawakilisha hoja na fikra zao bungeni bila kushaiwishiwa kwa rushwa.

CCM wakamatwa kwa rushwa
Katika hatua nyingine, viongozi watatu wa CCM, wanashikiliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa tuhuma za kujihusisha na vitendo vya rushwa kuhusiana na kura za maoni za marudio ndani ya chama hicho.
Kura za maoni zinatarajiwa kupigwa leo na wagombea wawili
walioongoza katika awamu ya kwanza ya kura za maoni zilizofanyika wiki iliyopita, Siyoi Sumari na Wililiam Sarakikya watapigiwa kura.

Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Arusha, Mbengwa Kasomambuto alithibitisha jana kwa simu kushikiliwa kwa viongozi hao ambao hata hivyo, alikataa kuwataja majina kwa sababu ya kiuchunguzi.

“Kweli tunawashikilia wana CCM watatu kwa mahojiano baada ya vijana wangu waliotapakaa kila sehemu ya Jimbo la Arumeru Mashariki kuwakuta katika mazingira yanayoashiria uwepo wa rushwa,” alisema...Soma zaidi www.mwananchi.co.tz

CHADEMA Na CCM Kama Republicans Na Democrats


Inavyoanza kuonekana kwa sasa vyama hivi pekee ndivyo vitakuwa vikimenyana kwenye              chaguzi kubwa.ni kama marekani.Naambiwa kule japo kuna vyama vingi sana vidogo hata vya kikomunisti,lakini nyote mnajua kuwa kwa karne sasa ni Republicans na Democrats pekee wanaotawala hasa siasa za nchi hiyo.Mwenendo ulivyo kwa sasa hapa nchini Ni CHADEMA na CCM. Tangu uchaguzi wa 2005 dalili hizi zilianza kuonekana hasa bungeni ambapo ungedhani kulikuwa na wabunge wa vyama hivyo pekee.japo CUF kiliongoza upinzani bungeni lakini kwa maoni yangu ni wabunge wa CHADEMA wale 11 waliojenga taswira ya upinzani.uchaguzi wa 2010 umeiweka CHADEMA kuwa Kambi rasmi ya upinzani pamoja na sarakasi za Hamad Rashid na Kafulila ambazo zilishindwa.
Mnaokumbuka tena katika chaguzi zote ndogo tangia 2005, ni CHADEMA na CCM ndo vimekuwa na ushindani wa kweli.Mnakumbuka kiteto,Tarime,Biharamulo,Busanda,Mbeya Vijijini,Igunga,Uzini,na sasa Arumeru? baadhi ya vyama vimekosa hata pumzi ya kuingia kwenye uchaguzi.
Kwa hiyo hakuna haja ya kuunganisha vyama vya upinzani kama ilivyokuwa inasemwa na baadhi ya watu hata wasomi.vyama vinaweza kuungana mkono tu na siyo kuungana.vilevile hakuna haja ya kuogopa kusajili vyama vipya kwani hata vikiwa 1000 itabaki kuwa CHADEMA Vs CCM.Kweli tunakoelekea ni kuzuri















Mwenyekiti wa chama cha Alliance for Democratic Change (ADC) Said Miraji (kushoto) na Katibu Mkuu wake, Kadawi Limbu wakionyesha rasimu ya Katiba ya chama chao na fomu za kuomba usajili wa muda kwenye ofisi ya Msajili wa Vyama vya siasa jijini Dar es Salaam jana.


Waliojitoa CUF waanzisha ADC



ALIYEKUWA Meneja wa Kampeni za Urais wa CUF mwaka 2010, Said Miraji na wenzake jana waliwasilisha rasmi kwa Msajili wa Vyama vya Siasa maombi ya usajili wa muda wa chama cha Alliance for Democratic Change (ADC).
Juzi, Miraji na aliyekuwa mgombea ubunge wa Temeke kwa tiketi ya CUF, Adawi Limbu walijitoa chama hicho na kutangaza kusudio la kusajili chama kipya.

Jana, ujumbe wa chama hicho uliwasili katika Ofisi ya Msajili, Dar es Salaam saa 7:30 mchana ukiongozwa na Miraji ambaye alijitangaza kuwa ni Kaimu Mwenyekiti na Katibu Mkuu wake, Limbu na kupokewa na Wangalizi wa Ofisi ya Msajili, Galasia Simbachawene.

Akizungumza na viongozi hao, Simbachawene alisema  kulingana na taratibu za usajili wa vyama,  maombi ya chama kabla ya kuwasilishwa kwa msajili yanahitaji kupatiwa muda ili yapitiwe na maofisa mbalimbali akiwemo Mwanasheria wa Ofisi ya Msajili.

“Nimepokea maombi. Msiwe wasiwasi yameshafika kwa Msajili. Utaratibu uliopo ni kwamba maombi yanapokewa na kupewa muda zaidi wa kuyapitia kwa kushirikiana na mwanasheria ili kuona kama yamekamilika baada ya hapo yatawasilishwa rasmi kwa Msajili,” alisema Simbachawene.

Vitu vilivyowasilishwa jana ni barua ya maombi ya usajili, rasimu ya katiba ya chama iliyoambatanishwa na hati ya kwenda kwa msajili (PF1) pamoja na hati ya kiapo ya kuwa chama cha jamii chini ya Sheria ya Vyama vya Siasa ya  mwaka 1992.

Miraji alisema wameamua kuanzisha chama hicho baada ya kutoona chama chochote cha siasa kinachowafaa  kujiunga akisema karibu vyote vinafanana tabia.

“Tumeamua kuanzisha chama cha siasa lakini, kitajikita kijamii zaidi.  Hatujafanya uamuzi wa kishabiki kwani siasa za nchi hii zilivyo, si rahisi mtu kutoka chama kimoja kwenda kingine kwani vyote vinafanana, vina maneno matamu sana hasa CCM ,” alisema Miraji.

Alisema ili kupata maoni ya wananchi kuhusu katiba ya chama hicho, rasimu ya katiba hiyo itaingizwa kwenye mitandao ya kompyuta pamoja na magazeti  na majarida na kusambazwa katika maeneo mbalimbali.
“Hatupo tayari kuwa na katiba ya mtu mmoja wala watu 100 tu, lazima tukusanye maoni ya muundo wa katiba kutoka kwa watu mbalimbali kupitia mitandao na kutoa matangazo kwenye magazeti yatakayoweza kuwafikia watu katika maeneo yote,” alisema Miraji.

Alisema katika katiba ya chama chao vitu walivyozingatia ni pamoja na ukomo wa madaraka na kuweka kamati maalumu ya usuluhishi ambayo haitawahusisha viongozi wa juu wa chama ili kuepeka kuwafukuza wanachama wanapofanya makosa ambayo yanaweza kurekebishika.

Kwa upande wake, Limbu alisema wananchi wanapaswa kuwa macho na vyama taasisi kwani viongozi wa vyama vya siasa wanafanya vyama hivyo kama mtaji.

“Chama hiki hakina mwenyewe watu wanaruhusiwa kuja kujiunga wasisubiri mpaka wafukuzwe katika vyama vingine ambavyo havijui umuhimu na thamani ya wanachama,” alisema Limbu.

Limbu aliwataka wanasiasa walio kwenye vyama visivyo na msimamo kuhamia chama hicho ili waweze kutetea haki za wananchi na kuwapa mwelekeo wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Walikitabiria kifo CUF
Walipokuwa wakitangaza kujitoa CUF, Miraji na mwenzake walikitabiria kifo cha chama hicho wakisema kimepoteza mwelekeo kutokana na kuongozwa na watu wanaodhani ni mali yao.

Pia walimshutumu Naibu Katibu Mkuu wa CUF Bara, Julius Mtatiro wakisema ameamua kwa makusudi kukiua.Hata hivyo, Mtatiro alijibu tuhuma hizo akisema, “Said Miraji ni mfuasi wa Hamad Rashid kwa muda mrefu sana.
Amekuwa akikihujumu chama yeye na Hamad Rashid, kuondoka kwake siyo tishio la CUF. Nafahamu anakwenda kukabidhiwa chama na Hamad Rashid kama kaimu mwenyekiti hadi Hamad atakamoliza ubunge wake, tunamtakia kila la heri katika kujitoa CUF.”


Siasa zetu za Tanzania zinatupeleka wapi?


Maswali ya kujiuliza ni mengi juu ya siasa za bongo.
Wengi watajiuliza tulipotoka ni wapi, tulipo ni wapi na ni wapi tunaelekea tukijua fika Tanzania ni nchi iliyobarikiwa kwa neema ya rasilimali watu na mali, lakini bado tu maskini wa fikra na tajiri wa rasilimali.
Blog hii inalengo kubwa na kutoa fursa ya kubadilishana mawazo wewe na watanzania wengine juu ya mstakabali wa siasa zetu na ni kwakiasi gani tutasaidiana kutoka hapa tulipo. Pamoja na hayo, kuangalia kwa undani aina ya siasa, uchumi na mipangilio ya kijamii ambayo, kama tutaipangilia, itatusaidia kufanya mipango ya kimaendeleo kwa uharaka na kuondoa umaskini uliokidhiri kwa kiasi cha watu kifikiria ni sehemu ya maisha yetu.
Tuwe na lengo la kutafuta njia za kusimamia siasa na taratibu za nguvu na mamlaka ambazo zitasaidia kufanya kazi kwa ufanisi zaidi yazilizopo. Tunataka kufanya hivyo kwa msingi wa umakinifu kwa yale yaliyofanyika vizuri kwa sasa na huko nyuma toka enzi ya Baba wa taifa, Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere, kufuatiwa na Mweshimiwa Ali-Hassan Mwinyi, Mweshimiwa Benjamin Mkapa na Mweshimiwa Raisi, Jakaya Mrisho Kikwete.
Karibu kwenye blog hii! Kazi yetu kubwa ndio hii inaanza, lakini tunapendelea kubadilishana mawazo, elimu, ujuzi, fikra na watu wenyewe uelewa mkubwa wa kufikiri na wahamasishaji ambao fikra zao zinashirikiana katika kuendeleza vizuri siasa za bongo, moja ya changamoto kubwa Tanzania

No comments:

Post a Comment