JAMII

Jamii Yaaswa Kuhusu Faida Za Utunzaji Miti


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira, Dk. Terezya Huvisa ameiasa jamii ya watanzania kujenga tabia ya kupanda na kutunza miti ili kufaidika na biashara ya hewa ukaa.
Dk. Huvisa ameyasema hayo mwishoni mwa wiki katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa alipofanya ziara ya kikazi kukagua miradi inayotekelezwa na Kampuni ya Green Resources katika vijiji vya Idete na Uchindile
Amezitaja faida za misitu kuwa ni uuzaji wa hewa ukaa ambayo kwa kiasi kikubwa hupatia wananchi fedha kwa ajili ya huduma muhimu za maendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa shule, zahanati, na kutoa ajira kwa jamii inayozunguka.
Dk. Huvisa amewasihi wananchi wa Mufindi kutumia utaalamu wa wawekezaji hao katika kuandaa mashamba yao ya miti na kudumisha uhusiano mzuri baina yao na wawekezaji. “msiuze ardhi yenu yote kwa wawekezaji bali tumieni fursa hiyo kuandaa mashamba yenu kitaalamu ili muweze kunufaika pia” Alisisitiza Dk. Huvisa.
Akitoa taarifa kwa Waziri, Meneja wa Mradi wa Green Resource Bw Sangito Sumari, amesema kiasi cha Shilingi bilioni moja zimetolewa na kampuni hiyo kusaidia miradi ya maendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Shule ya Awali, Barabara, na miradi ya Maji katika vijiji vya Idete, Mapanda, Uchindile, Makungu na Chogo.
Kuhusu biashara ya hewa ukaa katika mwaka 2010, “Kampuni imetoa asilimia kumi kwa ya mauzo ya hewa hiyo kwa vijiji vya wilaya ya Mufindi na Kilombero ambapo kijiji cha Chogo kilipata sh. Milion 10 , Mapanda milioni 30, Uchindile Milioni 75 na Kitete 10 milioni,” alisisitiza Bw. Sumari.
Kampuni ya Green Resources inafanya kazi zake  katika nchi ya Tanzania, Uganda na Msumbiji na inajishughulisha na upandaji wa miti, uvunaji wa hewa ukaa na mradi wa kuzalisha na kusambaza umeme unaandaliwa. 

No comments:

Post a Comment